Kama imekupita,hivi ndivyo ilivyokua kati ya Simba na Mwadui leo
‘Wekundu wa Msimbazi’ Simba wameshindwa kutamba
mbele ya timu ya Mwadui FC ya Shinyanga kwenywe mchezo wa kirafiki wa kujipima nguvu kuelekea mshikemshike wa ligi kuu Tanzania bara msimu ujao mchezo uliomalizika muda mfupi kwenye uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam.
Simba ikichezesha nyota wake wote wapya isipokuwa wale waliopo kwenye kikosi cha Taifa imejikuta ikishindwa kuonesha makali yake mbele ya wababe hao wa ligi daraja la kwanza msimu uliopita.
Kipindi cha pili Simba walijitahidi kuliandama lango la Mwadui lakini kukosa utulivu kwa washambuliaji wa Simba kuliwafanya waendelee kukosa magoli mengi kupitia nafasi nyingi walizozitengeneza, lakini safu ya ulinzi ya Mwadui inastahili pongezi kwa kiwango ilichoonesha kwenye mchezo wa leo kwa kuzuia mipira mingi ya mwisho ambayo iliyokuwa inawaendea washambuliaji wa Simba.
Kipindi cha kwanza kilimalizika huku timu zote zikiwa sare ya bila kufungana lakini zote zikiwa zimepoteza nafasi kadhaa za kufunga. Lakini kipindi chote hicho mpira ulikuwa ni wakawaida wenye mashambulizi mepesi kwa kila upande.
Mshambuliaji anayefanya majaribio kwenye klabu ya ‘Wekundu wa Msimbazi’ Simba, Papa Niang ambaye ni raia wa Senegal ameshindwa kutamba muda wote wa kipindi cha kwanza na kuonekana ni mchezaji wa kiwango cha kawaida na siyo kama ilivyokuwa ikidaiwa na msemaji wa klabu hiyo Haji Manara.
Kipindi cha pili timu zote zilianza kwa kufanya mabadiliko ya wachezaji lakini bado madiliko hayo hayakuzaa matunda kwa timu zote mbili.
Mwinyi Kazimoto, Hassan Kessy na Mussa Mgosi ni wachezaji wa Simba ambao kwa leo walionesha uhai mkubwa kwa upande wa Simba wakati Jabir Aziz Stima, Joram Mgoveke Julius Mropena na Shabani Kado wakiwa ni wachezaji waliocheza kwa kiwango cha juu kwa siku ya leo kwa upande wa Mwadui FC.
Wakati mpira unaelekea ukingoni, mlinda mlango wa Mwaui FC Shabani kado alitolewa nje kwa machela na baadae kukimbizwa hospitali baada ya kugongwa na wachezaji akiwa kwenye harakati za kuokoa mpira langoni kwake
Hadi mwamuzi wa mchezo huo anapuliza filimbi ya mwisho kuumaliza mchezo huo timu zote zilikuwa sare ya bila kufungana (0-0).
Kama imekupita,hivi ndivyo ilivyokua kati ya Simba na Mwadui leo
Reviewed by Steve
on
Monday, August 24, 2015
Rating:

No comments:
Post a Comment