Propellerads

Mkwasa azungumza haya kufuatia kukataliwa wachezaji wa Yanga, Azam




Kaimu Kocha Mkuu wa Taifa Stars, Charles Mkwasa ambaye ni kocha msaidizi wa
Yanga, amekerwa na kitendo cha klabu za Yanga na Azam kukataa kuwaachia wachezaji wao kwa ajili ya kujiunga na timu ya taifa inayojiandaa na mchezo wa kufuzu Kombe la Mataifa Afrika (Afcon) dhidi ya Nigeria.

Katika orodha ya wachezaji 28 walioitwa kuingia kambini ni Yanga na Azam pekee ambazo hazijaruhusu mchezaji yeyote kwa kile kilichohofiwa ni presha ya mchezo wa Ngao ya Jamii utakaopigwa Agosti 22, mwaka huu kati ya klabu hizo.
Aidha, Mkwasa amesema mbali na kwamba kukosekana kwa nyota hao kunaathiri programu zake, amepanga kutumia mchezo wa Ngao ya Jamii kupima viwango vya nyota aliowaita, iwapo hataridhishwa nao, atawapiga chini.
Katika hilo, Mkwasa amelazimika kuita nyota wengine 10 kutokana na Yanga na Azam kugomea kuachia wachezaji wao ambao tayari wapo kambini.

“Kwa namna moja ama nyingine, zimewakatalia wachezaji kutokana na presha ya mchezo wao (Ngao ya Jamii), hivyo nimeamua kuongeza wengine 10 ili kuwa na kikosi kipana ili tusipate tabu wakati wa mchujo wa mwisho kuelekea Uturuki.

“Ni kweli kuna athari kutokuwepo kwao maana kila kocha ana falsafa yake kiufundishaji, tunaamini kama tungekuwa nao kikosini ingesaidia kujua ‘fitness’ yao na kuendana na mfumo wangu, lakini ndiyo hivyo.

“Kwa upande mwingine mchezo wa Ngao ya Jamii utatusaidia kuangalia viwango vya wachezaji ambao wameshindwa kufika kambini kutokana na klabu zao kukataa, iwapo itaonyesha kuwa viwango vyao vipo chini kulinganisha na hawa tulionao kambini, basi tutaachana nao,” alisema Mkwasa.


Kikosi cha Stars kinatarajia kuondoka nchini Agosti 23, siku moja baada ya mchezo wa Ngao ya Jamii kuelekea Uturuki ambapo kitaweka kambi ya siku 10 kujiandaa na mchezo dhidi ya Nigeria utakaopigwa Septemba 5, mwaka huu.
Mkwasa azungumza haya kufuatia kukataliwa wachezaji wa Yanga, Azam Mkwasa azungumza haya kufuatia kukataliwa wachezaji wa Yanga, Azam Reviewed by Steve on Wednesday, August 12, 2015 Rating: 5

No comments:

Propellerads
Powered by Blogger.