Propellerads

Umeyasikia aliyosema Henry kuhusu Arsenal !!


                                                


LONDON, England
Unapoamua kuzungumza ukweli mara zote ni lazima utakuuma wewe unayezungumza au ukamuumiza yule au wale ambao unawasema, hasa kama ikiwa kwa mabaya au kwa
kukosoa.

Thierry Henry ana jina kubwa ndani ya Klabu ya Arsenal na kila shabiki wa timu hiyo analijua hilo, inaaminika kuwa ndiye mchezaji bora kuwahi kutokea ndani ya klabu hiyo, kwa ufupi heshima yake ni kubwa klabuni hapo.

Pindi alipotangaza kustaafu kucheza soka na kuamua kuwa mchambuzi, wengi waliamini kuwa ipo siku lazima atakwaruzana na timu yake hiyo ya zamani na ndivyo inavyoanza kutokea.
Awali alipoanza kazi ya uchambuzi ndani ya kituo cha Sky, hakuwa mkosoaji mzuri, lakini muda mfupi baadaye akaanza kukosoa mambo mengi yakiwemo hata yanayoihusu Arsenal.

Gumzo ni juu ya kauli yake kuwa Arsenal haiwezi kutwaa ubingwa kwa kumtegemea mshambuliaji Olivier Giroud, alisema anaamini ni jambo zuri kwa kocha wa timu hiyo, Arsene Wenger, kusajili straika wa kiwango cha juu kama kweli anahitaji ubingwa wa Premier.

                                            


Arsenal imekuwa ikipata tatizo la kutokuwa na straika daraja A kwa miaka mingi, angalau miaka ya hivi karibuni Wenger alikuwa akisajili wachezaji wa gharama kubwa tofauti na ilivyokuwa sera yake ya kutegemea chipukizi wa bei rahisi ili awakuze, ndiyo maana akapata taji la FA Cup na Ngao ya Jamii.

Giroud naye amemjibu Mfaransa mwenzake huyo na kuonyesha kupuuzia kile alichokisema, lakini akikaa chumbani kwake juu ya kitanda na kutulia, anaweza kuwa anaujua ukweli lakini tu hataki kuonyesha kuwa anaujua.

Kauli ya Henry, ambaye alifunga mabao 226 katika maisha yake ya Arsenal, ilikuwa hivi: “Nafikiri Giroud anacheza vizuri lakini unadhani unaweza kutwaa ubingwa kwa kumtegemea yeye? Sidhani kama inawezekana hiyo.”
Giroud, 28, anaelekea kumaliza msimu akiwa amefunga mabao 14 katika mechi 26 alizocheza baada ya kuwa nje kutokana na kuandamwa na majeraha kwa muda wa wiki kadhaa, hivyo kukosa mechi nyingi ndani ya msimu huu.

Arsenal inamaliza msimu huu ikiwa katika nafasi ya tatu nyuma ya Chelsea yenye Costa na Manchester City yenye Sergio Aguero, huku ikiwa mbele ya Manchester United yenye Robin van Persie na Radamel Falcao ambao hawakuwa kwenye kiwango kizuri.

Hali hiyo ya Falcao na van Persie inathibitisha kuwa ili ubebe ubingwa au ufanye vizuri, pamoja na kuwa na kikosi imara lakini straika wa kiwango daraja la kwanza na ambaye yupo kwenye kiwango kizuri ni muhimu zaidi.
Umeyasikia aliyosema Henry kuhusu Arsenal !! Umeyasikia aliyosema Henry kuhusu Arsenal !! Reviewed by Steve on Saturday, May 23, 2015 Rating: 5
Propellerads
Powered by Blogger.